Elimu kuhusu matumizi sahihi ya Vipimo na Ufungashaji Mkoa wa Njombe

Imewekwa:September 29, 2021

WAKALA WA VIPIMO YASISITIZA MATUMIZI YA VIPIMO SAHIHI MKOANI NJOMBE

Mkuu wa Mkoa wa Njombe Mhe. Marwa Rubirya ameipongeza taasisi ya Wakala wa Vipimo kwa uamuzi wa kutoa elimu kuhusu matumizi sahihi ya Vipimo na ufungashaji kwa Wakulima na viongozi mbalimbali wa Serikali kwani madalali Mkoani Njombe wamekuwa na tabia ya kuwanyonya wakulima kwa kuwalazimisha kununua mazao yao mashambani kwa kutumia Vipimo batili kama ndoo na Lumbesa.

Mhe, Rubirya amesema elimu ya Vipimo itasaidia Wakulima kuuza mazao ya kwa kutumia Vipimo sahihi vilivyohakikiwa ili mkulima aweze kunufaika kwa kupata fedha inayolingana na thamani ya mazao yake na kutaka vianzishwe vituo maalum kwa ajili ya kuuzia mazao na viewe na mizani iliyohakikiwa. Pia, ameitaka Wakala wa Vipimo kwa kushirikiana na taasisi zingine kukaa pamoja na kuhakikisha wanatoka na vifungashio ambavyo vinakubalika kwa nchi nzima hii itasaidia mazao yatakapofika sokoni yote kuwa na thamani sawa na ushindani utakao fanana kwenye soko.

Akizungumza na Mwandisi wetu Mhe. Balozi Dk. Pindi Chana Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Njombe ambaye Ofisi yake imeshirikiana na Wakala wa Vipimo kutoa mafunzo kuhusu matumizi sahihi ya Vipimo na Ufungashaji kwa Wakulima amesema, mpaka sasa Elimu ya Vipimo imetolewa katika Wilaya tatu ambazo ni Njombe Mjini, Wanging,ombe na Makete ambapo jumla ya Wajasiriamali na Wafanyabiashara 400 wamenufaika kwa kupata elimu kuhusu vipimo sahihi na namna ya kutambua kipimo kilicho hakikiwa.

Balozi Pindi chana amesema, elimu hii imekuja kipindi sahihi kwani suala la vipimo limekuwa changamoto hasa katika Mkoa wa Njombe ambapo Wananchi wanajihusisha na Kilimo cha Mahindi, Maharage, Parachihi na Viazi Mkulima analima kwa tabu kwa kutumia gharama kubwa lakini wanapokuja madalali kununua mazao wanalazimisha kununua kwa Vipimo batili vya Lumbesa na Visado hali inayosababisha mkulima kupata faida kidogo tofauti na ambavyo angeuza katika mzani angepata faida kubwa ndio maana tumeona kunahaja wakulima wapate elimu ya Vipimo na kufahamu faida za kuuza kwa kutumia mizani.

Kwa upande Wake Meneja wa Wakala wa Vipimo Mkoa wa Njombe Bw.Hennry Msambila amesema Wakala wa Vipimo hufanya uhakiki wa Vipimo mbalimbali katika Mkoa wa Njombe na mara baada ya ukaguzi mkuu hufanya kaguzi za kushtukiza katika maeneo mbalimbali ili kujiridhisha kama Vipimo hivyo vinatumika kwa usahihi kama vilivyohakikiwa awali. Pia, katika kuhakikisha Mkulima analindwa na kuuza mazao yake kwa kutumia Vipimo sahihi amehimiza Halmashauri zote kuhakikisha zinaanzisha maeneo maalumu ya kuuzia mazao na kuhakikisha wanaweka mizani iliyohakikiwa ili kuwasaidia Wakulima kuuza mazao yao kwa kutumia mizani hali ambayo itawasaidia Wakulima kupata fedha nyingi zitazoendana na mazao wanayouza.

Meneja Msambila amesema, Wakulima wanaouza mazao yao mashambani kwa kutumia vipimo batili wanaikosesha mapato Serikali na Halmashauri kwa kuto kukusanya ushuru halisi unaopaswa kulipwa. Vilevile amesema ufungashaji batili wa mazao kwa mtindo wa Lumbesa unadhohofisha ata afya za vibarua wanaokuwa wanabeba mizigo hiyo ambayo inakuwa na uzito mkubwa kinyume na Sheria ya Vipimo inavyoagiza.

Bi. Salome Benald ambaye ni Mkulima Wilaya ya Wanging’ombe ameeleza kuwa elimu aliyoipata kuhusu matumizi sahihi ya Vipimo na Ufungashaji imewafumbua sana macho watahakikisha wanawafikishia na wenzao ili wasiuze tena mazao yao kwa kutumia vipimo batili kama Lumbesa na Visado bali wajikusanye na kununua mizani zitakazo wasaidia kuuza mazao yao kwa kilogramu ili waweze kunufaika na mazao wanayolima kuliko kuwanufaisha Wafanyabiashara.