ELIMU YA MATUMIZI SAHIHI YA VIPIMO YATOLEWA KWA WABUNGE
Imewekwa:May 21, 2024Waziri wa Biashara na Maendeleo ya Viwanda Zanzibar Mhe. Omar S. Shaaban ameipongeza taasisi ya Wakala wa Vipimo (WMA) kwa namna inavyoendelea kusimamia usahihi wa vipimo katika sekta mbalimbali na kuhakikisha kunakuwa na haki baina ya pande mbili zinazofanya biashara.
Mhe.
Omar ameyasema hayo alipotembelea banda la Wakala wa Vipimo mara baada ya
kufungua maonesho ya wiki ya Viwanda na Biashara yanayofanyika katika viwanja
vya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania yakiwa na lengo la kutoa elimu kwa
waheshimiwa wabunge kuhusu majukumu na kazi zinazofanywa na taasisi zilizopo
chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara.
Kadharika,
Mhe. Omar Shaaban ameipongeza taasisi ya Wakala wa Vipimo Bara (WMA) kwa
kuendeleza mashirikiano na taasisi ya Wakala wa Vipimo Zanzibar (ZAWEMA) na kuahidi
kuendelea kutoa ushirikiano kwa taasisi hizo mara kwa mara ili kuhakikisha
zinatimiza lengo kuu ambalo ni kumlinda mlaji kupitia matumizi sahihi ya
vipimo.
Kupitia
maonesho hayo yaliyoandaliwa na wizara ya viwanda na Biashara waheshimiwa
wabunge mbali mbali wametembelea banda la wakala wa vipimo ambapo wamepata
kufahamu kwa undani majukumu ya taasisi hiyo hususani katika maeneo ya uhakiki
wa dira za maji na alama ambazo zinawekwa katika dira sahihi zilizohakikiwa,
Uhakiki wa mita za umeme ambapo ni eneo jipya ambalo limeanza kufanyiwa kazi,
pamoja na uhakiki wa pampu za kuuzia mafuta.
Vilevile,
Kaimu Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Vipimo Bw. Alban Kihulla ametoa elimu
kwa baadhi ya waheshimiwa wabunge kwenye eneo la ufungashaji wa mazao ya shamba
ambapo amewaeleza kuwa kwa mujibu wa sheria ya Wakala wa Vipimo Sura Na. 340
mazao yoye ya shamba yanatakiwa kufungashwa kwa uzito usiozidi kilogramu mia
moja (100 kg) na endapo gunia litafungashwa kwa uzito zaidi ya ule unaokubalika
kisheria hatua zitachukuliwa dhidi ya msafirishaji na mmiliki wa mzigo.
Vilevile,
katika maonesho yanayoendelea katika viwanja vya Bunge Kaimu Afisa Mtendaji
Mkuu Bw. Alban Kihulla amegawa zawadi ya picha yenye kaulimbiu ya maadhimisho
ya siku ya vipimo duniani kwa wageni mbalimbali waliofika kupata elimu kwenye
banda la wakala wa vipimo. Siku ya Vipimo Duniani imeadhimishwa katika mikoa
yote ya kivipimo Mei 20, 2024 ikiwa na kaulimbiu “Tunapima leo kwa kesho
endelevu” ambapo katika maadhimisho hayo wakala ilitoa mizani kwenye soko la Ilala
Jijini Dar es Salaam ili kuhamasisha matumizi sahihi ya vipimo na kuacha kupima
bidhaa kwa kutumia visado na makopo.
Wakala
wa vipimo inaendelea kuwasihi wafanyabiashara na wamiliki wote wa vipimo
kuhakikisha vipimo vyao vinakuwa sawa kila mara ili kutenda haki wakati wote
bila kuwapunja watumiaji wa huduma katika maeneo yao.