MKUU WA MKOA WA LINDI AHIMIZA MATUMIZI YA VIPIMO SAHIHI

Imewekwa:September 06, 2017

Mkuu wa Mkoa wa Lindi Mhe. Godfrey W. Zambi amewataka Wakala wa Vipimo Kuongeza nguvu zaidi katika kusimamia matumizi sahihi ya vipimo katika maeneo mbalimbali, ili wakulima na Wananchi kwa ujumla waweze kunufaika na mazao wanayolima pindi waendapo kuyauza wakati wa msimu.

Mkuu wa Mkoa ameyasema hayo alipotembelea banda la WMA, katika maonesho ya nane nane ambayo kitaifa yanafanyika katika mkoa wa Lindi kwenye viwanja vya ngongo. Pia amewataka Wakala wa Vipimo kushirikiana na maafisa waliopo katika ofisi ya mkuu wa mkoa katika kuhakikisha wakulima hawapunjwi pindi waendapo kuuza mazao yao. kwani baadhi ya wafanyabiashara wasio waaminifu, huchezea mizani yao kwa lengo la kuwapunja wakulima kwa lengo la kupata faida zaidi.

Vilevile Mhe. Godyfrey Zambi alielezwa na maafisa wa vipimo namna kangomba inavyowapunja wakulima, kwa kuwa siyo kipimo sahihi kinachopaswa kutumika kununulia mazao. Hivyo Wakala wa Vipimo inawapa wakulima elimu ya matumizi sahihi ya mizani iliyo hakikiwa. Pia wanaelekezwa namna ya kutambua alama zinazowekwa kwenye vipimo vilivyohakikiwa na Wakala ambazo ni stika maalum, pamoja na kugongwa nembo ya Taifa na tarakimu mbili za mwisho za mwaka husika. Mfano kwa mwaka huu 2017, itasomeka namba 17.

Akizungumza na mwandishi wetu baada ya ziara ya Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Afisa Vipimo wa Lindi Bw. Nyagabona Mkanjabi amesema, wamejipanga vizuri katika kusimamia matumizi ya vipimo sahihi na kuhakikisha mizani zote zinazotumika katika vyama vya ushirika vya msingi zinakaguliwa kabla ya misimu ya kuuza mazao kuanza. Pia watahakikisha kaguzi mbalimbali za kustukiza zinafanyika kipindi cha msimu wa kuuza mazao unapofika.

Pia, amewakaribisha viongozi wa vyama vya ushirika vya msingi pamoja na wananchi wote kutembelea banda la wakala wa vipimo katika maonesho ya nanenane mkoa wa Lindi na kujionea Mizani mbalimbali zinazopaswa kutumika katika ununuzi wa bidhaa mbali mbali na mazao ukiwemo mzani wa digital wa tani 2 ambao unapima bidhaa/mazao na kutoa risiti hapo hapo

Kaimu Meneja wa Wakala wa Vipimo Mkoa wa Lindi Bw. Andrew Mbwambo ametoa wito kwa Wakulima, wafanyabiashara na Wananchi wote kutojihusisha na vitendo vya kuchezea vipimo kwani kwa sasa adhabu ni kubwa baada ya Sheria ya Vipimo Sura namba 340 na Mapitio yake ya mwaka 2002 kufanyiwa marekebisho mwaka 2016.