MIZANI ZAIDI YA 225 IMEKAGULIWA KWA AJILI YA MSIMU WA UNUNUZI WA KAHAWA

Imewekwa:July 20, 2022

Wakala wa Vipimo (WMA) inaendelea na zoezi la ukaguzi wa mizani inayotarajiwa kutumika katika ununuzi wa zao la kahawa Mkoani Kagera. Ukaguzi huu hufanyika kila mwaka kabla ya kuanza kwa msimu wa ununuzi wa Mazao na mizani inayobainika kuwa sahihi uwekewa alama maalumu na Mkaguzi ambayo ni stika ya WMA na mizani yenye kasoro hukataliwa kutumika mpaka ifanyiwe marekebisho na fundi mizani mwenye lesseni kutoka Wakala wa Vipimo na mara baada ya matengenezo Mkaguzi hupita tena kukagua mzani kama upo sahihi unawekewa stika na kukubalika kutumika kununulia mazao.

Meneja wa WMA Kagera Bi. Harrieth Lukindo amesema, Mpaka sasa ukaguzi umefanyika katika Wilaya za Missenyi ambapo mizani 33 imekaguliwa, Muleba mizani 69 imekaguliwa, Bukoba mjini na Vijijini mizani 68 imekaguliwa pamoja na Wilaya ya Karagwe na Kyerwa ambapo zoezi bado linaendelea na mpaka sasa jumla ya mizani 60 imekaguliwa kwenye vyama vya msingi.

Kadharika, Meneja Harrieth amesema mara baada ya zoezi linaloendelea la kuhakiki mizani kukamilika msimu unapoanza wa kununua kahawa Wakala wa Vipimo hupita na kufanya ukaguzi wa kushtukiza kwenye vituo vya kununulia kahawa na kuhakiki kama mizani inatumika kwa usahihi kama ilivyohakikiwa. Endapo chama chohote cha Msingi kitajihusisha na uharibifu wa mizani hatua kali huchukuliwa dhidi yao kwa mujibu wa Sheria ya Vipimo Sura Na. 340 na Mapitio yake ya mwaka 2002.

Akizungumza wakati wa ukaguzi wa zoezi hilo Bi. Stella Kahwa ambaye ni Kaimu Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Vipimo alipokuwa Wilayani Kyerwa amesema kwamba msimu wa ununuzi wa Kahawa uanatarajiwa kufunguliwa kuanzia mapema mwezi Juni hivyo, ni lazima kuhakikisha vipimo vyote vitakavyotumika kwenye ununuzi wa Kahawa vinakaguliwa na mpaka sasa zoezi la ukaguzi linaendelea vizuri na limekamilika kwa asilimia 90 ambapo tunamalizia ukaguzi kwenye Wilaya za Karagwe na Kyerwa.