KAMATI YA BUNGE VIWANDA, BIASHARA NA MAZINGIRA YAIPONGEZA WAKALA WA VIPIMO

Imewekwa:November 18, 2022

KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE VIWANDA, BIASHARA NA MAZINGIRA YAIPONGEZA WAKALA WA VIPIMO KWA KUJENGA KITUO CHA UHAKIKI WA VIPIMO

Kituo cha Wakala wa Vipimo (WMA), Misugusuru Mkoa wa Pwani kimekuwa cha mfano na nchi za Afrika Mashariki zimekuwa zikija kujifunza ubora wa kazi zinazofanywa kwenye kituo hicho.

Kituo hicho kimekuwa kikitumika kuhakiki ujazo wa mafuta kwenye malori, kuhakiki mita za maji na umeme kilijengwa kwa gharama ya Shillingi bilioni saba.

Hayo yalisemwa jana na Naibu Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, Mhe. Exaud Kigahe (Mb), wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira, iliyotembelea kituo hicho.

Naibu Waziri alisema kituo hicho ni kipya na kimekuwa mfano bora kutokana na kazi zinazofanywa kiasi cha kuwavutia watu wa nchi jirani kuja mara kwa mara kujifunza kuhusu vipimo.

“Kituo hiki kinafanya kazi nzuri na kitaendelea kuwa mfano hivyo tunaamini mheshimiwa Rais ataendelea kutupa fedha tujenge vituo kama hivi kwa kanda kama ambavyo kamati ya Bunge imeshauri,” alisema Naibu Waziri Kigahe.

Kaimu Ofisa Mtendaji Mkuu wa (WMA), Bi. Stella Kahwa, alisema wabunge wameona hatua kubwa iliyofikiwa lakini wameshauri kuwe na maabara inayotembea ili kwenda kukagua mita za maji na umeme kwenye maeneo mbalimbali nchini.

Mwenyekiti wa Kamati Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira, Mhe. David Kihenzile alisema wameona namna mita za maji zinavyohakikiwa na zile za umeme kuhakikisha mwananchi anapewa mita ya maji au umeme yenye ubora ili alipe kile tu anachotumia.

Alipongeza utaratibu huo ambao alisema unamwezesha mwananchi kulipia kile ambacho anatumia na alishauri WMA iendelee kukagua mita hizo kuhakikisha zinakuwa na ubora wa hali ya juu ili kulinda maslahi ya mwananchi.

“Changamoto ambayo tumeiona ni kwamba hivi mtu anayetengeneza mita za maji Katavi au Shinyanga atazisomba zote aje zipimwe hapa Kibaha. Kwa hiyo tumewashauri wakala watazame haya mbeleni ikiwezekana vituo kama hivi vijengwe kwenye kanda lakini kwa kweli wanafanyakazi nzuri sana,” alisema