ELIMU KWA UMMA

Imewekwa:May 19, 2021

WAKALA WA VIPIMO YAENDELEA KUTOA ELIMU YA VIPIMO KATIKA MIKOA YA KUSINI

Wakala wa Vipimo (WMA) imeendelea kutoa elimu ya matumizi sahihi ya Vipimo kwa Wafanyabiashara, Wajasiriamali na Viongozi wa vyama vya msingi vya Ushirika (AMCOS) katika Mkoa wa Lindi. Elimu hiyo ni muendelezo wa kuhakikisha wananchi na wafanyabiashara wanafahamu majukumu ya taasisi hiyo na kufanya kazi zao kwa kuzingatia kanuni na Sheria ambazo zinasisitiza matumizi sahihi ya vipimo katika utoaji wa huduma mbalimbali na si matumizi ya vipimo batili kama kangomba.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mkutano wa elimu kwa umma Katibu Tawala Mkoa wa Lindi Bi. Rehema Madenge ambaye alimuwakilisha Mkuu wa Mkoa amesema elimu hiyo ya Vipimo imefika kwa wakati muafaka ambapo msimu wa ununuzi wa mazao unakaribia kuanza na alitumia wasaha huo kuwasihi viongozi wa vyama vya Msingi vya Ushirika kuhakikisha kuwa mizani zote zitakazotumiwa katika ununuzi wa mazao zihakikiwe na kuwekewa alama maalumu za Wakala wa Vipimo kama vile stika pamoja na Lakili (seal).

Bi. Rehema amewaeleza wafanyabiashara na viongozi wa vyama vya msingi kuwa wizi wa aina yeyote ni kosa la jinai hivyo hata kuibia wananchi na wakulima kwa kuchezea vipimo ni kosa la jinai na yeyote atakaye kamatwa kujihusisha na vitendo vya uchezeaji wa vipimo atakamatwa na kuchukuliwa hatua stahiki. “Nawasihi sana wanunuzi wa mazao kuacha kutumia vipimo batili kwakuwa kufanya ivyo ni kuwanyonya wakulima ndiomaana wafanyabiashara wanaendelea kwa kasi huku wakulima wanabaki katika hali duni ya kiuchumi itoshe kusema vitendo hivyo havikubaliki imefika wakati mkulima inabidi apate tija kunufaika na kile anachokizalisha kwa kuuza mazao kwa kutumia vipimo sahihi (mzani)” Katibu Tawala Mkoa wa Lindi alieleza.

Kadhalika, Bi. Rehema Madenge ameipongeza Wakala wa Vipimo kwa kuendelea kupanua wigo wa kazi za vipimo katika maeneo mapya ambapo kwa sasa taasisi hiyo inafanya uhakiki wa dira za maji pamoja na mita za umeme, kwa kuzingatia hilo Bi. Rehema ameagiza Mamlaka ya maji Mkoa wa Lindi Luwasa kuhakikisha wateja wote wapya na wazamani wanafungiwa mita za maji zilizohakikiwa na Wakala wa Vipimo na kuwekewa alama maalumu ambayo ni lakiri (seal).

Akizungumza na mwandishi wetu Meneja wa Wakala wa Vipimo Mkoa wa Lindi ndugu, Andrew Mbwambo amesema kuwa Wakala wa Vipimo inatekeleza majukumu yake kwa mujibu wa Sheria ya Vipimo Sura Na. 340 na mapitio yake mbalimbali hivyo, mizani za wafanyabiashara wadogo na zile zitumikazo katika vyama vya msingi vya ushiriki kwa kawaida hufanyiwa uhakiki mara moja kwa mwaka na mara baada ya kumaliza kaguzi mbalimbali za kushtukiza hufanyika katika maeneo hayo ili kujiridhisha kama vipimo vinatumika kwa usahihi kama vilivyohakikiwa awali.

Meneja Mbwambo amewaonya wafanyabiashara na viongozi wa vyama vya msingi vya ushirika kujiepusha na vitendo vya uchezeaji wa vipimo kwa lengo la kutaka kujipatia faida zaidi kwani kufanya hivyo ni kinyume cha Sheria ya Vipimo Sura na. 340 na mapitio yake mbalimbali ambayo inaeleza adhabu kwa mtu atakaye kutwa amechezea vipimo ni faini isiyopungua shilingi laki moja (100,000/=) na isiyozidi millioni ishirini (20,000,000/=) inategemea na ukubwa wa makosa.

Vilevile, wakati wa mafunzo wafanyabiashara na Viongozi wa AMCOS walielezwa madhara mbalimbali yatokanayo na matumizi yasiyo sahihi ya vipimo ambayo ni pamoja na kukiuka Sheria ya Vipimo ambayo inaweza kusababisha mfanyabiashara au Chama cha Ushirika kuadhibiwa kwa kulipa faini au kupata adhabu ya kifungo mahakamani na mali yake kutaifishwa. Pia, kumuibia mteja kwa kumpunja ni moja wapo ya wizi na nikinyume na maandiko ya vitabu vitakatifu, lakini vilevile biashara zinaweza kufa ama kufirisika kwa kuzidisha bidhaa kwa wateja pasipo kutumia vipimo vilivyo sahihi katika biashara.

Akizungumza na mwandishi wetu baada ya kupata mafunzo hayo Bw. Abubakari Mbalala ambaye ni kiongozi wa Mnacho AMCOS amewapongeza sana Wakala wa Vipimo kwa kuwapatia elimu kuhusu matumizi ya vipimo sahihi kwani na wao kama viongozi wataenda kulisimamia na kuhakikisha katika msimu huu unaotarajia kuanza hivi karibuni mizani zote zitakazotumika zitakuwa zimehakikiwa na zitatumika kwa usahihi ili kuepuka kuwapunja wakulima wa zao la korosho na ufuta. Pia, wameiomba wakala wa vipimo kuendelea kutoa semina za vipimo mpaka wilayani ili kuwafikia watu wengi zaidi ili waweze kupata kuelewa namna ya kutumia vipimo sahihi.

Meneja wa Wakala wa Vipimo Lindi Bw. Andrew Mbwambo ametoa wito kwa watumiaji wote wa vipimo kuzingatia matumizi sahihi ya vipimo na endapo wataitaji ushauri wa kitaalamu wasisite kutembelea ofisi za wakala wa vipimo zilizopo Mtaa wa Elieti au kupiga namba ya simu ya bure 0800 110097.