Elimu kwa Umma kwenye viwanja vya Maisara Zanzibar

Imewekwa:December 09, 2021

WAKALA WA VIPIMO TANZANIA BARA NA ZANZIBAR WALISHIRIKIANA KUTOA ELIMU KUHUSU MATUMIZI SAHIHI YA VIPIMO KWENYE MAONESHO YA 6 YA BIDHAA ZA VIWANDA.

Wakaazi wa Zanzibar wamehimizwa kujitokeza kwa wingi kwenye Viwanja vya Maisara kwa lengo la kupata elimu kuhusu matumizi sahihi ya Vipimo. Elimu ya Vipimo inatolewa kwa ushirikiano wa taasisi mbili ambazo ni Wakala wa Vipimo Tanzania Bara (WMA) na Wakala wa Vipimo Zanzibar (ZAWEMA).

Akizungumza na mwandishi wetu Mkurugenzi wa Vipimo Zanzibar Bw. Mohammed Mwalim Simai amesema, kwa mujibu wa Sheria ya Vipimo Wakala wa Vipimo ndio taasisi pekee inayosimamia matumizi sahihi ya vipimo kwa kuhakikisha kuwa vipimo vinavyotumika katika biashara viko sahihi, ili kuwalinda walaji na watumiaji wa vipimo. Kuzingatia matumizi sahihi ya vipimo kutaepusha madhara yatokanayo na vipimo batili.

Wananchi wakitembelea banda la Wakala wa Vipimo watapata kufahamu majukumu yanayotekelezwa na taasisisi hiyo ikiwa ni pamoja na kufanya uhakiki wa vipimo mbalimbali kama vile mizani inayotumika kwenye maduka ya kuuzia nyama na bidhaa mbalimbali za majumbani, kutoa ushauri wa kitaalamu kwa watumiaji wa vipimo, kudhibiti vipimo vinavyotumika na vivavyopaswa kutumika katika biashara. Alisema Mkurugenzi Mohammed.

Akizungumza na mwandishi wetu meneja wa Wakala wa Vipimo Kitengo cha Bandari Tanzania Bara Bw. Peter Chuwa ameeleza, Wakala wa Vipimo kadhalika inasimamia usahihi wa kiasi cha mafuta yanayoingia nchini kwa njia ya Meli ili kuhakikisha kiasi cha mafuta kilichoagizwa na Serikali kinapokelewa kikiwa sahihi. Lakini pia, uhakiki unafanyika katika flow meters zinazotumika kupokelea mafuta ambapo uhakiki wake hufanyika kila baada ya miezi kumi na mbili ili kujiridhisha usahihi wake. Vilevile, Wakala wa Vipimo inahakiki matenki makubwa ya yanayotumika kuhifadhia mafuta (fixed storage tanks), uhakiki wa matenki ya malori yanayotumika kusafirisha mafuta ambayo pia huhakikiwa mara moja kila baada ya miezi kumi na mbili (12).

Meneja chuwa kadhalika amesema, uhakiki hufanyika kwenye vituo vya kujazia mafuta kwa kuhakiki pampu zinazotumika kujaza mafuta kwenye vituo vyote vya kuuzia mafuta, pampu zikihakikiwa na kuwa sahihi huwekewa alama maalumu ya utambuzi ambayo ni stika maalumu inayoonesha pampu hiyo kuwa imehakikiwa. Pia, uhakiki hufanyika kwenye visima vya kuhifadhia mafuta ardhini (Underground tanks), matenki hayo uhakikiwa mara moja kila baada ya miaka mitano (5).

Wakala wa vipimo kadhalika, imepata wasaa wa kuwatembelea wajasiriamali mbalimbali kwenye maonesho ya bidhaa za Tanzania na kuangalia bidhaa zinazozalishwa na kufungaswa na wajasiriamali wandani. Baadhi ya wazalishaji wa bidhaa hizo wamefungasha vizuri bidhaa zao na kuweka alama za vipimo kwa usahihi, wajasiriamali ambao wamefungasha bidhaa bila kuzingatia matumizi sahihi ya vipimo, wamepatiwa elimu ya namna bora ya kufungasha bidhaa na namna sahihi za kuandika alama za vipimo kwenye bidhaa zao kwa lengo la kuongeza thamani ya bidhaa wanazozalisha ili ziweze kushindana kitaifa na kimataifa.

Mkurugenzi wa Vipimo Zanzibar Bw. Mohammed Simai ameeleza kuwa, Wakala wa Vipimo itaendelea kutoa huduma bora kwa kuwalinda watumiaji wa vipimo kwa kuingia katika maeneo mapya ya utendaji kazi, kama inavyofanyika sasa upande wa Wakala wa Vipimo Tanzania Bara, ambao wameanza kufanya uhakiki wa mita za maji zote zinazoingizwa katika matumizi na uhakiki wa mita za umeme. Uhakiki wa mita za umeme na maji upande wa Tanzania bara unafanyika katika kituo cha uhakiki kilichopo kibaha Misugusugu mkoa wa Pwani, Kilimanjaro na vituo vya uhakiki vilivyojengwa katika baadhi ya mikoa ya Wakala wa Vipimo bara. Hivyo, kwa hatua waliyoipiga Wakala wa VipimoTanzania bara na upande wa Zanzibar tunajijengea uwezo ili tuweze kuingia kwenye usimamizi wa vipimo kwenye maeneo hayo mapya ili wananchi wapate huduma sahihi kulingana na thamani ya fedha yao.

Mkurugenzi Mohammed amemalizia kwa kueleza kuwa endapo vipimo vitasimamiwa kwa usahihi itasaidia Serikali kukusanya kodi kwa usahihi kutoka katika bidhaa mbalimbali zinazozalishwa nchini na bidhaa zinazoingizwa kutoka nje ya nchi. Kadhalika vipimo visipo simamiwa kwa usahihi itasababisha wananchi kupunjwa na kupata huduma au bidhaa ambazo haziendani na thamani ya fedha wanayotumia.

Mkurugenzi Mohammed ametoa wito kwa Wananchi na wafanyabiashara wote wa Tanzania bara na Zanzibar kuhakikisha wanatumia vipimo sahihi na endapo watakutana na changamoto yoyote inayohusu vipimo wafike kwenye ofisi za Wakala wa Vipimo kwa ajili ya kupata msaada wa kitaalamu. Wamiliki wa vipimo wameonywa kutochezea vipimo kwa lengo la kuwaibia wananchi, kwani kufanya hivyo ni kosa kisheria na hatua kali zitachukuliwa dhidi ya wote watakaobainika kufanya vitendo hivyo ambavyo vinakatazwa hata kwenye maandiko matakatifu.