SETI 25 ZA VIPIMO VYA MAWESE ZAGAWIWA KWENYE MAADHIMISHO YA SIKU YA VIPIMO DUNIANI MKOANI KIGOMA
Imewekwa:May 21, 2023
Wakala wa Vipimo imeadhimisha siku ya Vipimo Duniani Mkoa wa Kigoma kwa kugawa jumla ya seti za vipimo 25 zenye ujazo wa lita 5, lita 10 na lita 20 kwa lengo la kuhimiza matumizi ya vipimo sahihi wakati wa uuzaji na ununuzi wa mawese na kuachana na matumizi ya vipimo batili maarufu kama bidoo ambayo huwanyonya na kuwapunja wakulima wakati wa mauzo.
Maadhimisho
ya Siku ya Vipimo Duniani huadhimishwa kila mwaka ifikapo mwezi Mei tarehe 20
na Kaulimbiu ya maadhimisho haya kwa mwaka 2023 ni Vipimo katika kuwezesha mfumo wa usambazaji wa chakula duniani.
Jumla
ya vikundi vya Wakulima ishirini na nne (24) vimepatiwa vipimo hivyo ambapo
Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Vipimo Bi. Stella Kahwa ameziomba halmashauri
za Mkoa wa Kigoma kuona haja ya kutenga fedha na kununua vipimo vingine ili
kuwasaidia wakulima kuuza mawese kwa kutumia vipimo sahihi na kutekeleza
kampeni ya kutokomeza matumizi ya vipimo batili inayosema “bidoo sasa basi”.
Bi.
Stella ameeleza kuwa jukumu la kusimamia haki katika biashara ambalo lipo
katika Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara linatekelezwa na Wakala wa
Vipimo ikiwa ni taasisi mwanachama wa Shirika la Vipimo Duniani (OIML) Shirika
ambalo hutoa miongozo mbalimbali kuhusiana na Vipimo baada ya kufanya tafiti za
kisayansi. Ameeleza kuwa mwaka 1875 nchi mbalimbali zilikutana nchini Ufaransa
na kwa pamoja waliamuwa kuweka mlingano ili kipimo kitachotumika katika nchi
moja kiwe sawa sawa na kipimo kitachotumika katika nchi nyingine ndio maana
hata vipimo tulivyoleta na kukabidhi kwenye maadhimisho haya vina usahihi wa
hali ya juu na vimewekewa alama maalumu uhakiki ambayo ni muhuri wa bibi na
bwana.
Kwa
upande wake Mgeni Rasmi Mhe. Kanali Isack Mwakisu Mkuu wa Wilaya ya Kasulu
ambaye alimuwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Geita Kamishna Jenerali Mstaafu wa Jeshi
la Zima Moto na Uokozi Mhe. Thobias Andengenye ameupongeza uongozi wa Wakala wa
Vipimo kwa kuchagua kufanya maadhimisho Kitaifa kwenye Mkoa wa Kigoma na kwa
kuona umuhimu wa kutengeneza vipimo seti 25 ambavyo vimegawiwa kwenye vikundi
mbalimbali vya Wakulima kwa ajili ya kuhimiza matumizi sahihi ya Vipimo na
kuachana na Vipimo batili maarufu kama bidoo.
Kanali
Mwakisu ameeleza kuwa vipimo vinatumika kwa namna mbalimbali kwenye maisha yetu
ya kila siku na katika shughuli za kilimo vipimo hutumika kuanzia uandaaji wa
shamba, kupanda mbegu, umwagiliaji, uwekaji wa mbolea shambani hadi wakati wa
uvunaji na usambazaji wa mazao. Ameeleza kuwa vipimo ni nyenzo muhimu ambayo
hutumika wakati wa kuuza hata wakati wa kusafirisha mazao kutoka sehemu moja
hadi nyingine hivyo, wakulima wote wanapaswa kuzingatia matumizi sahihi ya
vipimo kwenye mfumo mzima wa uzalishaji na usambazaji wa chakula.
Kwa
upande wake Bi. Amina Mohamed ambaye ni mkulima na muuzaji wa mawese Wilaya ya
Buhigwe amesema vipimo walivyopatiwa vitawasaidia kuuza mawese kwa kutumia
vipimo sahihi siyo tena kwa njia ya ndoo kwani wanunuzi walikuwa wanawapunja
kwa kutaka kujaziwa mawese kwenye ndoo kwa ujazo wa hadi kufikia kumwagika
kitendo ambacho kilikuwa kinawasababishia hasara kubwa na kumnufaisha mnunuzi.