WAFANYABIASHARA WA SOKO LA MAWENZI MKOANI MOROGORO WAHIMIZWA KUTUMIA VIPIMO SAHIHI
Imewekwa:September 01, 2023
Meneja wa Wakala wa Vipimo (WMA) Mkoa wa Morogoro Bw. Phanuel Matiko amewataka viongozi wa masoko ya Mkoa wa Morogoro na wafanyabiashara wa masoko yote hususani soko la Wakulima Mawenzi kuzingatia matumizi sahihi ya vipimo wakati wote na kujiepusha na matumizi ya vipimo batili ambavyo havikubaliki Kisheria kama makopo, visado na madebe kwenye uuzaji wa mazao na bidhaa mbalimbali.
Wito
huo umetolewa kwenye kikao kilichofanyika kwenye soko la wakulima Mawenzi na
kuwahusisha viongozi wa masoko ya Fire, Chamwino, Mazimbu, Kihonda Maghorofani,
Nane Nane, Kingalu, Mji Mpya, Bigwa pamoja na wafanyabiashara wa soko la mawezi
na viongozi wa Serikali za Mtaa.
Meneja
Matiko ameeleza kuwa lengo la Wakala wa Vipimo ni kuhakikisha kunakuwa na usawa
wakati wa ununuzi na uuzaji wa bidhaa mbalimbali kwa kuhakikisha muuzaji
anapata pesa anayostahili na mnunuzi anapata bidhaa kulingana na thamani ya
fedha yake pasipo kupunjwa. Kadhalika, amesisitiza kuwa Wakala wa Vipimo jukumu
lake kuu ni kumlinda mlaji na kuhakikisha kunakuwa na mazingira wezeshi ya
kufanya biashara pasipo kuwa na malalamiko kutoka upande wowote na sikukwamisha
biashara kufanyika.
Vipimo
batili maarufu kama visado, ndoo na Madebe vinaikosesha Serikali takwimu sahihi
na vilevile havitendi haki kwakuwa visado vinatofautiana ujazo na hatua kali za
Kisheria zitachukuliwa kwa wote watakao bainika kuendelea kuvitumia kama
vipimo.
Matiko
amesema ni muda wa wafanyabiashara kubadilika kwa kuanza kutumia mizani sahihi
na iliyohakikiwa katika uuzaji wa bidhaa zao na wanunuzi kutokukubali kununua
bidhaa bila kupimiwa kwenye mizani kila mara wanapoenda kupata huduma kwenye
masoko.
Kwa
upande wake Meneja wa Soko la Mawenzi Bw. Abdul Mkangwa amewataka wafanyabiashara
wa soko hilo kutii Sheria bila shuruti na kuwahimiza wafanyabiashara wote wa
soko hilo kuhakikisha wanakuwa na mizani sahihi iliyohakikiwa ili kujiepusha na
usumbufu wa kutozwa faini pale wanapokutwa na makosa ya kutumia vipimo batili
kwani kutumia vipimo hivyo ni kosa Kisheria.