WAKALA WA VIPIMO (WMA) YASHIRIKI KUTOA ELIMU SOKO LA KARUME MACHINGA COMPLEX

Imewekwa:May 18, 2024

Kuelekea katika maadhimisho ya siku ya Vipimo Duniani,Wakala wa vipimo (WMA) imeshiriki katika kutoa elimu juu ya matumizi sahihi ya vipimo kwa wafanyabiashara wa soko la karume machinga complex wilayani ilala Jijini Dar es salaam.

Akitoa elimu hiyo katika mkutano wa robo ya tatu ya mwaka kwa wafanyabiashara hao, meneja wa mkoa wa vipimo wa ilala Bwana Mhono Nashon, amewajengea ufahamu wa namna ya kutumia vipimo sahihi vilivyo hakikiwa na Wakala wa Vipimo katika maeneo yao ya biashara ili kuleta usawa baina ya mfanyabiashara na mnunuzi.

Bwana Nashon ameongeza kuwa wakala wa vipimo itaendelea kuwatembelea wadau mbalimbali katika maeneo yao ya biashara na kuwapa elimu juu ya masuala mbalimbali ya vipimo ili kuondokana na ufanyaji biashara usiozingatia sheria na taratibu za vipimo.

“Tunatakiwa kutumia vipimo sahihi na vilivyohakikiwa na Wakala wa Vipimo ili kuepuka madhara yatokanayo na upimaji usiozingatia taratibu na sheria za vipimo, natoa rai kwa wafanyabiashara katika soko hili la karume machinga complex, kuondokana na upimaji wa kimazoea kwa kutumia mafungu, visado, vifungashio na vipimo vinginevyo batili kwani hii inadumaza ustawi wa biashara, lakini pia kutengeneza uwiano usio sawa baina ya mfanyabiashara na mteja na hivyo kudumaza maendeleo ya taifa katika Nyanja mbalimbali” amesema Bwana Nashon.

Kwa upande wake meneja wa soko hilo Bi.Stella Mgumia, ameishukuru Wakala wa Vipimo kwa ushiriki wake katika mkutano huo na wafanyabiashara sanjari na kutoa elimu ya matumizi sahihi ya vipimo katika maeneo mbalimbali ya biashara.

Bi. Mgumia amesema kuwa, wafanyabiashara katika soko la karume machinga complex wameahidi kutumia vipimo sahihi katika maeneo yao ya biashara na kutoa ushirikiano kwa wakala hiyo katika kazi zake.

Wakala wa Vipimo (WMA) inaendelea kujikita katika kutoa elimu juu ya matumizi sahihi ya vipimo na kuwafikia wadau katika maeneo mbalimbali ili kuwajengea ufahamu juu ya masuala mbalimbali ya vipimo. Wakala hii inaendelea kuchangamana na wananchi na wadau katika muundo chanya kwa nyakati mbalimbali huku ikijiandaa na maadhimisho ya siku ya Vipimo Duniani ambayo hufanyika Mei 20 ya kila mwaka.

Wakala wa Vipimo (WMA) na taasisi zingine za vipimo za kikanda na duniani kote zitaadhimisha siku ya vipimo duniani huku kauli mbiu ikiwa ni “tunapima leo kwa kesho endelevu”.