WAKALA WA VIPIMO YA ADHIMISHA SIKU YA VIPIMO DUNIANI KWA KUGAWA MIZANI SOKO LA ILALA.
Imewekwa:May 31, 2024
Wakala wa Vipimo (WMA) imeungana na taasisi zingine za vipimo duniani kuadhimisha Siku ya Vipimo ambayo huadhimishwa Mei 20 kila mwaka.
Wakala
wa Vipimo imeadhimisha siku ya vipimo duniani (World Metrology Day) kwa kutembelea
soko la ilala na kutoa elimu juu ya matumizi sahihi ya vipimo katika maeneo
mbalimbali ya biashara sanjari na kugawa mizani iliyohakikiwa na Wakala wa
Vipimo kwa makundi ya wafanya biashara sokoni hapo.
Akimuwakilisha
Mkuu wa Wilaya ya Ilala Mhe.Edward Jonas Mpogolo katika hafla ya utoaji elimu
na ugawaji wa mizani ilyofanyika sokoni hapo,Katibu Tawala wa wilaya hiyo
Bi.Charangwa Seleman Makwiro ameipongeza Wakala wa Vipimo kwa kuwa na utaratibu
wa kuwatembelea wadau na wafanya biashara na kuwapa elimu juu ya matumizi
sahihi ya vipimo katika maeneo yao ya biashara.
Aidha,Bi.Charangwa
amewaasa wafanya biashara sokoni hapo kujenga tabia endelevu ya kutumia mizani
iliyohakikiwa na Wakala wa Vipimo katika biashara zao ili kuepuka madhara
yatokanayo na matumizi yasiyo sahihi ya vipimo.
“
Ndugu zangu wafanyabiashara, upimaji wa bidhaa zenu kwa kutumia visado ambavyo
mnaviita take away, na vipimo vingine vya mafungu na hata vifungashio, sio
vipimo halali na vya uhakika, tunatakiwa tutumie vipimo sahihi kama vile mizani
iliyohakikiwa na Wakala wa Vipimo ili kuepuka kujiibia na kupata hasara pamoja
na kudumaza hali ya biashara zetu. Nawaasa mkiwa na jambo lenu mnahitaji
utatuzi ofisi za Wakala wa Vipimo zipo, nendeni mtashughulikiwa na kutatuliwa
shida zenu zote zinazohusu matumizi sahihi ya vipimo” amesema Bi.Charangwa.
Sanjari
na hayo Bi.Charangwa ameshiriki kugawa mizani iliyohakikiwa na Wakala wa Vipimo
kwa baadhi ya makundi ya wafanya biashara ili kuwasaidia katika shughuli
mbalimbali za biashara na kuleta chachu ya matumizi sahihi ya vipimo katika
maeneo ya biashara.
Naye
Meneja wa Mkoa wa Vipimo wa Ilala Bwana Mhono Nashon ametoa elimu juu wa
matumizi sahihi ya vipimo na kujibu hoja mbalimbali zilizowasilishwa kwake na wafanyabiashara.
Bwana
Nashon amewataka wafanya biashara kujenga utamaduni wa matumizi sahihi ya
vipimo na kuondokana na upimaji holela wa bidhaa kwani upimaji huo unafifisha
ustawi wa biashara na kudumaza maendeleo ya taifa.
“
Ofisi yetu ya Wakala wa Vipimo Mkoa wa Ilala ilifanya utafiti mdogo tu wa
kivipimo, tulinunua karoti, tulipimiwa kwa kutumia visado tofauti ambapo
tulipopeleka kwenye vipimo tulikuta kisado kimoja kina kina kilogram 3.8 na
kingine kina kilogram 4, sasa hapa utaona ni jinsi gani mfanya biashara
anavyojidhulumu” amesema Bwana Nashon
Kwa
upande wake mwenyekiti wa wafanya biashara wa soko la Ilala Bwana Ali Karimu
Mbiku, ameshukuru Wakala wa Vipimo (WMA) kwa kutoa elimu juu ya matumizi sahihi
ya vipimo pamoja na kuwapa mizani iliyohakikiwa na Wakala hiyo.
Bwana
Mbiku ameiomba Wakala kuendelea kushirikiana na wafanya biashara na kuwapa
elimu na kuwakumbusha mara kwa mara juu ya matumizi sahihi ya vipimo na
kuchochea maendeleo ya taifa.
Wakala wa Vipimo na taasisi zingine za vipimo duniani zinaadhimisha siku ya vipimo ambayo hufanyika Mei 20 kila mwaka ikiwa ni kumbukizi ya mkataba wa kimataifa uliosainiwa mwaka 1875 Jijini Paris, nchini Ufaransa. Mkataba huo ulisainiwa na mataifa 17 kwa lengo la kuweka mfanano na usawa wa vipimo duniani ambapo Tanzania ilisaini mkataba huo Julai 17, 1964. Maadhimisho ya Siku ya Vipimo Duniani mwaka huu yamepambwa na kauli mbiu isemayo “tunapima leo kwa kesho endelevu”