WAKALA WA VIPIMO YAENDELEA KUTOA ELIMU KUHUSU MIZANI KWA WAKULIMA WA PAMBA

Imewekwa:April 22, 2018

WAKALA WA VIPIMO YAENDELEA KUTOA ELIMU KUHUSU MIZANI KWA WAKULIMA WA PAMBA

Wakala wa Vipimo (WMA) inaendelea na zoezi la utoaji elimu kwa Wakulima na wadau wa zao la pamba katika Mikoa saba (7) ya Kanda ya Ziwa ambayo ni Mwanza, Geita, Simiyu, Tabora, Shinyanga, Mara pamoja na Kagera. Jumla ya wilaya 27 zitapata elimu ya Mizani sahihi zinazotakiwa kutumika wakati wa msimu wa kuuza pamba.

Lengo kuu la kutoa elimu kwa Wakulima kuhusu Mizani sahihi zinazopaswa kutumika katika msimu wa ununuzi wa pamba, ni kumlinda Mkulima ili apate fedha anayostahili kulingana na uzito wa pamba anayoiuza, pia kuhakikisha mkulima anajua mambo muhimu ya kuzingatia ili kumuwezesha kutambua mizani sahihi na zilizo hakikiwa na pia kuweza kutambua kwa urahisi mizani zilizochezewa au kuharibiwa/kuharibika

Zoezi hili la elimu ya Mizani kwa Wakulima wa pamba ni zoezi endelevu ambalo hutolewa na Wakala wa Vipimo kila mwaka kabla ya kuanza kwa msimu wa ununuzi wa zao hilo, na mpaka sasa zaidi ya mizani 626 imeanza kuhakikiwa tayari kwa maandalizi ya msimu wa ununuzi wa pamba.

Mara baada ya zoezi la elimu kukamilika kwa Wakulima wa pamba WMA itaingia katika zoezi la awamu ya pili, ambalo ni operation maafisa vipimo watapita katika vituo vya ununuzi wa pamba na kufanya kaguzi za kushtukiza ili kuhakiki usahihi wa mizani zinazotumika na zinavyotumika.

Mkulima wa pamba ataweza kutambua mizani zilizohakikiwa na Wakala wa Vipimo kwa kuzingatia vitu vifuatavyo; Kwanza, Mizani zilizo hakikiwa zinakuwa na lakili (seal) yenye ngao ya taifa pamoja na tarakimu mbili za mwisho za mwaka husika ambapo kwa mwaka 2018 itasomeka (18).

Pili, mizani zilizohakikiwa zinakuwa na stika maalum ya WMA ambayo inaonesha tarehe mizani iliyokaguliwa na tarehe ya mwisho kutumika, Vilevile Mkulima anatakiwa kuhakikisha kuwa mizani inasoma sifuri (0) kabla hajaweka pamba yake kwa ajili ya kuipima.

Kwa mujibu wa Sheria ya Vipimo sura na. 340 na mapitio yake ya mwaka 2002 imeelezea faini za makosa mbalimbali ambapo kwa mkosaji wa kosa la awali akipelekwa Mahakamani akakutwa na hatia adhabu ni faini isiyopungua 300,000 na isiyozidi millioni 50 au kifungo kisichozidi miaka miwili (2) au vyote kwa pamoja.

Vilevile, endapo mchezea vipimo atakamatwa na kosa kwa mara ya pili na kuendelea na akipelekwa Mahakamani akakutwa na hatia adhabu ni faini isiyopungua 500,000 na isiyozidi millioni 100 au kifungo kisichozidi miaka mitano (5) au vyote kwa pamoja.

Pia, endapo mtuhumiwa atakamatwa na kukubali kosa lake basi atafifilishwa ambapo faini yake ni kiasi cha fedha kisichopungua 100,000 na isiyozidi millioni 20.

Wakala wa Vipimo inatoa wito kwa wadau wote wa zao la pamba kujiepusha na vitendo vya udanganyifu wa aina yeyote haswa uchakachuaji wa mizani wakati wa ununuzi wa pamba, kwani kwa yeyote atakaye kamatwa kwa makosa hayo atashitakiwa kwa mujibu wa sheria.

Pia, WMA ina namba maalumu kwa ajili ya wananchi kupiga na kupata msaada pindi wakutanapo na changamoto za kivipimo, namba hiyo ni 0800 110097 namba hii ni bure kabisa.