WAKALA WA VIPIMO YAPONGEZWA KUTOA ELIMU YA VIPIMO SONGEA

Imewekwa:August 26, 2021

Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Mhe. Pololet Kamando Mgema ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Songea ameipongeza taasisi ya Wakala wa Vipimo (WMA) kwa kutoa mafunzo ya matumizi sahihi ya Vipimo na namna bora ya kuzingatia ufungashaji sahihi wa bidhaa kwa Wafanyabiashara, Wajasiriamali na Wakulima wa Mkoa wa Ruvuma na ameitaka taasisi hiyo kuendelea kuwasaidia wafanyabiashara kwa kuwapa elimu ya vipimo mara kwa mara na kufanya kaguzi za kushtukiza ili kujiridhisha kama vipimo vinatumika kwa usahihi.

Kadhalika Mhe. Pololet Kamando Mgema ameipongeza Wakala wa Vipimo kwa kuongeza na kupanua wigo wa kazi za vipimo katika maeneo mapya ambapo kwa sasa taasisi hiyo inafanya uhakiki wa dira za maji pamoja na mita za umeme, kwa kuzingatia hilo Mhe. Pololet ameagiza Mamlaka zote za maji Mkoa wa Ruvuma Ruwasa na Souwasa kuhakikisha wateja wote wanafungiwa mita za maji zilizohakikiwa na Wakala wa Vipimo.

Vilevile, amewaonya wafanyabiashara wa Mkoa wa Ruvuma kuacha tabia ya kutumia vipimo batili kama ndoo, dumla, lita, makopo na visado na badala yake watumie mizani sahihi ambayo imehakikiwa na Wakala wa Vipimo kwani kwa kufanya hivyo itawasaidia kutojipunja na wao kutowapunja wateja wao hivyo kujenga uaminifu Zaidi katika biashara. Mhe. Pololet Mgema ameyasema hayo jana wakati akifungua mafunzo na elimu kwa umma kuhusu matumizi sahihi ya Vipimo na ufungashaji kwa wafanyabiashara wa Mkoa wa Ruvuma yaliyofanyika katika ukumbi wa Manispaa ya Songea.

Akiwasilisha mada mtaalamu kutoka Wakala wa Vipimo Bi. Rehema Michael aliwaeleza wafanyabiashara hao kuwa Wakala wa Vipimo ni Wakala ya Serikali ambayo inatekeleza majukumu yake kwa mujibu wa Sheria ya Vipimo Sura Na. 340 (mapitio ya mwaka 2002). Lengo la Wakala wa Vipimo ni kumlinda mlaji na umma kwa ujumla kwa kufanya yafuatayo: Kuhakiki vipimo vinavyotumika kwenye Sekta za Biashara, Afya, Usalama na Mazingira,Kudhibiti matumizi yasiyo sahihi ili kuilinda jamii iweze kuepukana na madhara yatokanayo na matokeo ya matumizi na upimaji usio sahihi katika Biashara, Afya, Usalama na Mazingira.

Vilevile, Wakala wa Vipimo husimamia matumizi sahihi ya vipimo kwa njia ya kufanya ukaguzi wa mara kwa mara (scheduled and surprise inspections), Kukagua bidhaa zilizofungashwa (prepacked goods) toka nje ya nchi na zile zinazozalishwa hapa nchini, Kuidhinisha aina mpya ya vipimo vinavyoagizwa toka nje ya nchi na vinavyoundwa hapa nchini (pattern approval), Kutoa ushauri wa kitaalamu kuhusiana na vipimo, Kutoa vibali vya Ugezi na leseni za ufundi na uundaji wa vipimo mbalimbali, Kuiwakilisha nchi Kikanda na Kimataifa katika masuala ya vipimo.

Meneja wa Wakala wa Vipimo Mkoa wa Ruvuma ndugu Nyagabona Mkanjabi aliwahasa wafanyabiashara hao kujiepusha na vitendo vya uchezeaji wa vipimo kwa lengo la kutaka kujipatia faida zaidi kwani kufanya hivyo ni kinyume cha Sheria ya Vipimo Sura na. 340 na mapitio yake mbalimbali ambayo inaeleza adhabu kwa mtu atakaye kutwa amechezea vipimo ni faini isiyopungua shilingi laki moja (100,000/=) na isiyozidi millioni ishirini (20,000,000/=) kwa kosa. Hivyo, wito umetolewa kwa watumiaji wote wa vipimo kuzingatia matumizi sahihi ya vipimo na wafanyabiashara hao wameaswa kutembelea ofisi za wakala wa vipimo zilizopo katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma kwa ajili ya kupata ushauri wa kitaalamu kuhusu vipimo au kutoa maoni na kuwasilisha malalamiko yao ili yaweze kufanyiwa kazi kwa lengo la kuboresha utoaji huduma bora kwa Wananchi.

Pamoja na hayo wafanyabiashara walielezwa madhara mbalimbali yatokanayo na matumizi yasiyo sahihi ya vipimo ambayo ni pamoja na kukiuka Sheria ya Vipimo ambayo inaweza kusababisha mfanyabiashara kuadhibiwa kwa kulipa faini au kupata adhabu ya kifungo mahakamani na mali yake kutaifishwa. Pia, kumuibia mteja kwa kumpunja ni moja wapo ya wizi na nikinyume na maandiko ya vitabu vitakatifu, lakini vilevile biashara zinaweza kufa ama kufirisika kwa kuzidisha bidhaa kwa wateja pasipo kutumia vipimo vilivyo sahihi katika biashara.

Akizungumza na mwandishi wetu mshiriki wa mafunzo hayo ndugu Mathew ambaye ni mfanyabiashara wa gesi songea amewapongeza sana Wakala wa Vipimo kwa kuwapatia elimu ya matumizi ya vipimo sahihi kwani itawasaidia sana ili kuepuka kujipunja na kuwapunja wateja wao na kuhakikisha wanatumia mizani mkatika uuzaji na ununuzi wa bidhaa mbalimbali na amewataka zaoezi ilo liwe endelevu mara kwa mara.