WAZIRI JAFO AKABIDHI MAGARI MATANO KWA WAKALA WA VIPIMO
Imewekwa:February 27, 2025
Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Dkt. Selemani Jafo (Mb) amekabidhi magari matano kwa taasisi ya Wakala wa Vipimo ikiwa ni sehemu ya kuendelea kuboresha utoaji wa huduma za uhakiki na ukaguzi wa vipimo bidhaa zilizofungashwa kwa haraka na kwa wakati kwa Wananchi ambao ndio watumiaji wa vipimo na bidhaa kila siku.
Kadhalika,
Mhe. Dkt. Selemani Jafo ameelekeza magari hayo yakatumike katika kaguzi
mbalimbali za bidhaa zilizofungashwa kwa kuhakikisha vipimo vinakuwa sahihi
katika bidhaa za nondo na mabati kwa kusimamia usahihi wa vipimo ili mnunuzi wa
mwisho aweze kupata bidhaa inayoendana na thamani ya fedha anayolipa.
“Wananchi
wananunua nondo kiasi kwamba hata majengo yao yanakuwa hatarini kwakuwa wazalishaji
wanasema wanazalisha nondo za mm 16 lakini zinakuwa chini ya vipimo hivyo, sasa
niagize wazalishaji wote wa nondo kuzalisha nondo zenye ubora na zenye vipimo
sahihi halikadhalika kwa wazalishaji wa mabati.” Amesema Waziri Jafo.
Waziri
Jafo ameielekeza wakala wa Vipimo kuendelea kufanya kaguzi za kushtukiza kwenye
viwanda vya uzalishaji wa bidhaa za nondo na mabati ili kuhakikisha bidhaa
zinazofika kwenye masoko zinakuwa na vipimo sahihi kwa lengo la kuwalinda
wanunuzi wa bidhaa hizo ili kuepukana na uchezewaji wa vipimo.
Bw.
Alban Kihulla Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Vipimo amemshukuru Waziri wa
Viwanda na Biashara kwa kuja kukabidhi magari matano ambayo yatasaidia kufika
katika maeneo mbalimbali kwa ajili ya kutoa huduma za usimamizi na ukaguzi wa
vipimo.
“Mhe.
Waziri wa Viwanda na Biashara katika mwaka huu wa fedha 2024/25 Wakala ilipanga
kununua magari saba lakini mpaka sasa tumepokea magari matano ambayo
umetukabidhi siku ya leo na magari mengine mawili yatafika hivi karibuni na
gharama ya magari hayo matano ni Bil. 1,004,739,000.”
Bw. Alban amesema Wakala wa Vipimo itaendelea kutoa huduma za usimamizi wa vipimo kwa wakati kwa lengo la kuwalinda watumiaji wa huduma hizo na kaguzi mbalimbali za kushtukiza zitaendelea kufanyika ili kuhakikisha bidhaa zinazoingia kwenye masoko zinakuwa na vipimo sahihi na adhabu kali zitachukuliwa kwa mujibu wa Sheria ya Vipimo Sura Na. 340 kwa wazalishaji watakaobainika kuchezea vipimo.