WMA ILALA YATEKELEZA MKAKATI WA ELIMU MASOKONI KWA KILA MDAU

Imewekwa:June 25, 2024

WAKALA WA VIPIMO MKOA WA ILALA YATEKELEZA MKAKATI WA ELIMU MASOKONI KWA KILA MDAU

Wakala wa Vipimo Mkoa wa Ilala imetekeleza mpango mkakati wake wa utoaji wa elimu juu ya matumizi sahihi ya vipimo na ufungashaji wa mazao kwa usahihi kwa mujibu wa Sheria ya Vipimo.

Zoezi hilo la utoaji wa elimu, limefanyika katika soko la Ilala ambapo maafisa vipimo kwa kushirikiana na viongozi wa soko wamepita katika kila ghala, kitalu na maeneo yote ya biashara sokoni hapo na kutoa elimu ya matumizi sahihi ya vipimo na kuwajengea ufahamu juu ya Sheria mbalimbali za Vipimo.

Zoezi hilo la utoaji elimu kwa wadau na wafanyabiashara masokoni ni endelevu ambapo Maafisa Vipimo wa Mkoa wa kivipimo wa Ilala watapita katika kitalu, ghala na sehemu mbalimbali za biashara na kutoa elimu ya matumizi sahihi ya vipimo kwa kila mdau na mfanyabiashara.

Aidha, Meneja wa Mkoa wa Kivipimo wa Ilala Bw.Muhono Nashon amekutana na kufanya kikao na viongozi wa kamati ya soko la buguruni katika ofisi za Wakala wa Vipimo Mkoa wa Ilala.

Katika kikao hicho, Bw. Nashon amewaasa Viongozi hao wa soko la Buguruni kuwafikishia ujumbe wafanyabiashara kutoka Wakala wa Vipimo juu ya matumizi sahihi ya vipimo na kuwa mabalozi wazuri katika maeneo yao ya biashara.

Sanjari na hayo, Bw. Nashon ameweka mikakati ya ushirikiano chanya baina ya viongozi hao na WMA katika kutokomeza ufungashaji holela wa mazao (lumbesa) na udhibiti wa matumizi yasiyo sahihi ya vipimo katika maeneo mbalimbali ya biashara kama matumizi ya makopo na visado.

Huku hayo yakijiri, Bw. Nashon ameendelea na mapambano dhidi ya ufungashaji holela wa mazao (lumbesa) ambapo amefanikiwa kukamata na kuliweka kizuizini gari lenye namba za usajili T790 DLC kwa kosa la kupakia mazao yaliyofungashwa katika uzito wa zaidi ya kilogramu 100 (lumbesa) na kukiuka Sheria ya Vipimo.

Bw. Nashon amesema kuwa ukamataji huo umetokana na kaguzi za kushitukiza zinazofanywa na WMA katika nyakati mbalimbali kwa kupita katika maghala, vitalu na njia za usafirishaji ili kubaini ufungashaji wa mazao hayo.

Bw.Nashon ameongeza kuwa mmiliki wa gari hilo na wahusika wote katika ufungashaji huo holela (lumbesa) watachukuliwa hatua za kisheria kwa mujibu wa Sheria ya Vipimo.